Saturday, July 7, 2012

Mgomo wa madaktari na kuthaminiwa kwa wasomi


Mgomo huu wa madaktari wa mwaka 2012 ambayo sasa iko katika awamu ya tatu imejadiliwa kwa kirefu na kwa kiina na wengi na mimi sitapenda kutoa chanzo, sababu nk. Ila ningependa kuongelea mada moja ambayo nimeshawahi  kuigusia kwenye blog hii ya IMHO inayohusu utawala wa walio wa kati au uwezo mdogo. Kwa kifupi wale wenye ujuzi na uwezo huwekwa pembeni katika mfumo ambao upo sasa wa kiutawala na uendeshaji kwa ujumla.
Lakini kibaya zaidi mufmo mzima unaonekana kutothamini usomi na ujuzi. Tukiwasikiliza kwa makini madaktari, walimu na wasomi wengine – tunasikia wakisema “sisi mshahara wetu ni …. Na mbunge ambaye hata hajamaliza darasa la saba anapata milioni 10” Tunaweza kuleta mjadala mkubwa kuhusu sentensi hii na kuwaita waroho, au tukawaambia hakuna kinachowasimamisha kugombea ubunge. Lakini tukifanya hivyo tutakuwa hatujaelewa kile kilichojificha katika sentensi hii.
Katika dunia ya leo hasa hapa nchini – tunaweka thamani ya mtu kwa kupima kipato chake. Huu ni ukweli tupende tusipende. Mara ngapi unasikia watu wanasema “Mtu anajiona wa maana kumbe anapanda daladala” . Au “Fulani anajisikia, kumbe anaishi ….” Sentensi kama hizi zinaonyesha wazi kwamba ili ukubalike kuwa una mafanikio katika jamii yetu tunatarajia mtu awe na gari na anaishi maeneo Fulani, akivaa nguo za aina Fulani nk. Kwa kifupi jamii yetu imebadilika na hivi sasa tumekuwa nchi ya walaji (Consumer society) ingawa kama nchi hatuzalishi kile tunachotamani (hatuna viwanda vya magari, nguo, nk). Sasa basi kumiliki gari, nyumba, mavazi etc yanahiitaji pesa. Hivyo kama daktari anashindwa kuendesha Range Rover Vogue, lakini mfanyabiashara aliyeishia darasa la saba akiweza, je hii ni kusema tutamheshimu zaidi mfanyabiashara? Inaelekea ndivyo madaktari wanavyoona. Na kwa Bahati mbaya kwa kuwaambia “kama hamjaridhika ondokeni” – imekuwa kama kuwathibitishia imani yao hii.
Ni vyema tukianza kuthamini watu kwa UJUZI wao na si kwa MALI zao. Kumiliki gari kubwa au nyumba kubwa inaweza ikakufanya uishi kwa starehe zaidi lakini haikuongezi akili au ujuzi. Na pia kama jamii tuache dharau kwa watu. Hata kama mtu hamiliki mali nyingi, tuthamini vipaji, ujuzi na elimu yao. Lakini muhimu zaidi, muda umefika mfumo wote uanze kuthamini kwa pesa na kuwazawadia wale wenye ujuzi na si kuwajali ‘wajanja’.
Utatuzi wa mgomo huu na kutoridhika kwa wasomi ni suala ambalo ni vyema sote tukaitafakari na tukianza kubadilika kimawazo – Change Tanzania!